Mwaniaji ugavana kaunti ya Kilifi na mbunge wa Malindi Aisha Jumwa, gavana wa kaunti ya Lamu anayetafuta kuhifadhi kiti chake Fahim Twaha na Mike Mbuvi Sonko gavana wa zamani wa Nairobi anayetafuta ugavana wa Mombasa ni miongoni mwa wanasiasa 25 ambao uadilifu wao unatiliwa shaka na wametajwa kutofaa kuwania nyadhifa za uongozi.

Hii ni baadha ya Muungano wa makundi mbali mbali yanayolenga uadilifu kwa jina National Integrity Alliance – NIA kupitia kwa kampeni inayoitwa “The Red Card Capaign” kutoa orodha ya majina ya wanasiasa ambao uadilifu wao unatiliwa shaka ukishikilia msimamo kwamba hawafai kuwania nyadhifa za uongozi.

Muungano huo wa uadilifu unajumuisha shirika la Transparency International Kenya – TI-Kenya, lile la Inuka Kenya Ni Sisi!, Mzalendo Trust, The Institute for Social Accountability (TISA) na tume ya haki za binadamu yaani Kenya Human Rights Commission -KHRC. Orodha hiyo ina jumla ya majina 25 ambayo ni;

1. Aisha Jumwa – Mwaniaji ugavana kaunti ya Kilifi na mbunge wa Malindi
2. Ali Korane – Gavana wa kaunti ya Garissa anayetafuta kuchaguliwa tena
3. Anne Waiguru – Gavana wa kaunti ya Kirinyaga anayetafuta kuchaguliwa tena
4. Babu Owino – Mbunge wa Embakasi Mashariki anayetafuta kuchaguliwa tena
5. Cleophas Malala – Seneta wa kaunti ya Kakamega anayewania ugavana
6. Daniel Manduku – Mwaniaji ubunge wa Nyaribari Masaba
7. Didmus Barasa – Mbunge wa Kimilili anayetafuta kuhifadhi kiti chake
8. Evans Kidero – Gavana wa zamani wa Nairobi anayewania ugavana Homa Bay
9. Fahim Twaha – Gavana wa kaunti ya Lamu anayetafuta kuhifadhi kiti chake
10. Godhana Dhadho Gaddae – Gavana wa kaunti ya Tana River anayetafuta kuchaguliwa tena.
11. Johanna Ng’eno – Mbunge wa Emurrua Dikir anayetafuta kuhifadhi kiti chake
12. John Walukhe – Mbunge wa Sirisia anayetafuta kuchaguliwa tena
13. Joseph Samal – Mbunge wa Isiolo Kaskazini anayetafuta kuchaguliwa tena.
14. Kembi Gitura- Mwaniaji ugavana kaunti ya Muranga
15. Lilian Omollo – Mwaniaji useneta kaunti ya Embu
16. Mathew Lempurkel – Mbunge wa zamani wa Laikipia kaskazini anayewania wadhifa huo
17. Mike Mbuvi Sonko – gavana wa zamani wa Nairobi anayetafuta ugavana wa Mombasa
18. Mohamed Abdi Mohamud – gavana wa kaunti ya Wajir anayetafuta kuhifadhi kiti hicho
19. Muthomi Njuki – Gavana wa kaunti ya Tharaka Nithi anayetafuta kuhifadhi kiti chake.
20. Oscar Sudi – Mbunge wa Kapseret anayetafuta kuhifadhi kiti chake
21. Phillip Kaloki – Mwaniaji mwenza wa Ugavana kaunti ya Nairobi
22. Rigathi Gachagua – Mwaniaji mwenza wa urais wa muungano wa Kenya Kwanza
23. Samson Cherargei – Seneta wa sasa wa kaunti ya Nandi anayetaka kuchaguliwa tena
24. Samuel Arama – Mbunge wa Nakuru Mjini magharibi anayetaka kuchaguliwa tena
25. Sospeter Ojaamong’ – Mwaniaji ubunge wa Teso kusini na gavana wa sasa wa kaunti ya Busia.

Muungano wa NIA umetoa orodha hiyo kwenye kikao na wanahabari leo Jumapili ambapo umeelezea kwamba umekuwa ukifuatilia maadili ya viongozi kulingana na sura ya sita ya katiba na kubaini kwamba wapo wanasiasa wenye maadili ya kutiliwa shaka ambao wanawania nyadhifa za kuchaguliwa.

NIA ilifafanua kwamba walio kwenye orodha yao wamewahi kutajwa na mashirika mbali mbali au kufikishwa mahakamani kwa makosa kama vile ufisadi, matumizi mabaya ya mamlaka, uhalifu wa kiuchumi na mengine.

Muungano huo umeweka kesi mahakamani kutafuta ufafanuzi wa kiwango cha chini zaidi cha uadilifu ambacho wawaniaji nyadhifa za kuchaguliwa wanastahili kudhihirisha.