Mwendesha mashtaka mkuu wa Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu ICC Karim Khan, amesema jana kuwa mahakama hiyo itaanzisha uchunguzi kuhusu uwezekano wa uhalifu wa kivita unaofanywa na Urusi nchini Ukraine.

Katika taarifa, Khan amesema kuwa anatangaza maamuzi yake ya kuanzisha uchunguzi kuhusiana na hali nchini Ukraine haraka iwezekanavyo.

Khan amesema baada ya kupitia uchunguzi wa awali wa hali hiyo, ameridhika kwamba kuna sababu za kimsingi za kuamini kwamba madai yote ya uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya binadamu vimefanyika nchini Ukraine katika matukio kabla ya uvamizi wa Urusi.

Khan ameongeza kuwa kwa kuzingatia kupanuka kwa mzozo huo katika siku za hivi karibuni, ni nia yake kwamba uchunguzi huo pia utajumuisha madai yoyote mapya ya uhalifu yaliyo chini ya mamlaka ya ofisi yake ambayo yatafanywa na pande yoyote katika mzozo huo katika eneo lolote la Ukraine.

 Kwa Hisani:Dw Swahili